Sunday 1 November 2015

NITA TEKELEZA AHADI ZOTE ASEMA MBUNGE WA MBEYA VIJIJIN

Mbunge mteule wa Jimbo la Mbeya Vijijini kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Oran Njeza, ameahidi kutekeleza ahadi zote alizozitoa wakati wa kampeni zikiwamo zilizitolewa na wagombea udiwani kupitia  chama hicho walioshindwa.

Njeza alitoa ahadi hizo juzi akiwa katika mji mdogo wa Mbalizi, muda mfupi baada ya kukabidhiwa hati ya ushindi na kuwaonyesha wapiga kura wake.

Aliwataka wananchi kumpa ushirikiano wakati atakapoanza kutekeleza ahadi hizo, huku akidai kuwa atahakikisha kila kilichoahidiwa na mgombea udiwani wa CCM ambaye hakushinda pia kinatekelezwa.

“Kuna baadhi ya wagombea wa nafasi za udiwani kupitia chama chetu katika kata mbalimbali za jimbo hili ambao kura hazikutosha, lakini natambua kuwa waliahidi vitu vingi vizuri kwa ajili ya maendeleo ya jimbo letu, nawaahidi kuwa nitazitekeleza zote hata kwa kutumia rasilimali zangu binafsi” alisema Njeza.

Alisema yeye atafanya kazi bila kuwabagua wananchi wa jimbo hilo kwa namna yoyote ile huku akiwataka madiwani wote walioshinda kupitia vyama vingine vya siasa kushirikiana naye katika shughuli za maendeleo ya jimbo hilo bila kujali itikadi za vyama vyao.

Aliongeza kuwa atahakikisha katika miaka yote atakayofanya kazi kama mbunge, watu wa Mbeya vijijini wanabadili maisha yao kwa kuboresha huduma za jamii ikiwamo huduma za afya na maji.

Aidha, alisema kuwa atahakikisha wananchi wa jimbo hilo wanapatiwa pembejeo za kilimo ikiwamo mbolea ya ruzuku kwa wakati ili waweze kuboresha kilimo na kuwa na uhakika wa chakula na ziada kwa ajili ya biashara.

Alisema ushuru na michango isiyokuwa ya lazima atahakikisha inaondolewa ili watu wafanye maendeleo mengine ya familia zao kutokana na mapato wanayopata kwenye kilimo na biashara ndogo ndogo wanazofanya.

Njeza aliwataka wananchi kuanza maandalizi ya kuunda vikundi kwa ajili ya kupatiwa mikopo iliyoainishwa kwenye Ilani ya CCM inayoelekeza kuwa kila kijiji kitapatiwa Sh. milioni 50, kwa ajili ya wanawake na vijana, ili iwe rahisi kuzipata kwa kukopeshwa punde fedha hizo zitakapoanza kutolewa.

Katika hatua nyingine mbunge huyo aliwataka wananchi kuacha kufanya mambo ambayo yanaweza kusababisha uhasama miongoni mwao, huku akiahidi kujenga upya misingi ya CCM aliyodai kuwa imebomolewa na watu anaowatuhumu kuwa ni wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), katika kata ya Nsalala wakati wanashangilia ushindi wa diwani wa chama chao.

No comments:

Post a Comment