Uamuzi wa kufuta uchaguzi huo ulitangazwa jana majira ya saa 7.45
mchana na Mwenyekiti wa Zec, Jecha Salim Jecha, ambaye alizungumza na
waandishi maalum katika ofisi ya tume hiyo iliyopo Maisara na baadaye
taarifa hizo kutangazwa na Kituo cha Televisheni cha Shirika la
Utangazaji Zanzibar (ZBC).
Jecha alisema vikwazo vilivyojitokeza katika uchaguzi huo ndivyo
vilivyochelewesha utoaji wa matokeo ya uchaguzi ndani ya wakati
uliopangwa kisheria na kwamba ndicho kilichoifanya Zec kuamua kufuta
matokeo yote ya uchaguzi katika majimbo 54 ya Zanzibar.
Alisema kuna sababu tisa zilizosababisha kufikia uwamuzi huo
ikiwamo wajumbe ndani ya tume kufikia hatua ya baadhi yao kuvua mashati
na kuanza kupigana na wengine badala ya kuwa makamishna wa tume walikuwa
ni wawakilishi wa vyama vyao wakati kuna vyama vingi vilivyoshiriki
uchaguzi huo, ambavyo havikupata fursa ya kuwa na makamishna ndani ya
tume na vinashiriki uchaguzi mkuu.
“Kumegundulika kasoro nyingi katika uchaguzi huu miongoni mwa hizo,
kubainika kwa baadhi ya vituo hasa Pemba vimekuwa na kura nyingi kuliko
Daftari la Wapigakura,” alisema mwenyekiti huyo.
Aidha, alisema wamepokea taarifa kutoka kisiwani Pemba kuwa
kulifanyika uhamishaji wa masanduku ya kura na kuhesabiwa eneo la nje ya
vituo kitendo ambacho ni kinyume cha taratibu za sheria za uchaguzi,
pamoja na mawakala wa Chama cha Tadea kutolewa nje ya vituo wakati zoezi
la upigaji kura likifanyika katika majimbo mbalimbali kisiwani Pemba.
Mwenyekiti huyo alisema Zec imeridhika kuwa kuna vituo vilivamiwa
na vijana kuonekana kuandaliwa na vyama vya siasa na kufanya fujo
ikiwamo kupiga watu na kuzuiwa watu kufika katika vituo vya kupigia kura
kutimiza haki yao ya kikatiba.
“Vyama vya siasa vimeonekana kuingilia majukumu ya tume ikiwamo
kujitangazia ushindi na kusababisha mashinikizo kwa tume, na kumekuwapo
na malalamiko mengi yanayoashiria kutoridhika na mchakato mzima wa
upigaji kura, kuhesabu na kutoa matokeo ya uchaguzi huo,” alisema Jecha.
Aidha, alisema kuna fomu za matokeo ya vituo vingi vya Pemba namba
zake zimefutwa na kuandikwa upya juu yake, kitendo ambacho kinaonesha
kulikuwa na lengo la kufanya udang’anyifu kwa matokeo yaliojazwa katika
fomu hizo.
“Kwa kuzingatia hayo na mengine, sijayaeleza mimi nikiwa mwenyekiti
wa tume ya uchaguzi Zanzibar, nimerizika kwamba uchaguzi huu haukuwa na
haki na kunaukiukwaji mkubwa wa sheria na taratibu za uchaguzi, hivyo
kwa uwezo nilionao natangaza rasmi matokeo yote yamefutwa na kunahaja ya
kurudia uchaguzi huu,”alisema.
Wakati mwenyekiti huyo akitoa maamuzi hayo makamishna wawili wa
tume ya uchaguzi kutoka Chama cha Wananchi (CUF), Nassor Khamis Mohammed
na Ayoub Bakari Hamad, wamemtaka rais wa Zanzibar aunde tume ya majaji
ya kumchunguza mwenyekiti wa tume hiyo kwa sababu ameshindwa kutekeleza
kazi yake aliyopewa kwa kuzingatia katiba na sheria.
Alisema tume hiyo iwapo itathibitika mwenyekiti huyo ameshindwa
kufanya kazi, achukuliwe hatua ikiwamo kuondoshwa katika wadhifa huo kwa
vile kitendo alichofanya cha kutangaza maamuzi hayo bila ya
kuishirikisha tume ni uvunjaji mkubwa wa sheria wa tume ya uchaguzi
ambayo inatakiwa itoe maamuzi baada ya kushauriana na akidi ya wajumbe
ya kutoa maamuzi iwe imekamilika.
“Mwenyekiti kafuta matokeo bila ya kuwapo majadiliano hayo ni
maamuzi yake binafsi na sio maamuzi ya tume, hatujawahi kujadili na
kupitisha uamuzi kama huo tangu wananchi wakamilishe kazi ya kupiga
kura,”alisema Ayoub.
Kamishna Zec aipinga
Bakari Hamad kamishna wa tume hiyo, alisema kwa mujibu wa matokeo
yote yaliokusanywa, yanaonesha hakukuwa na tatizo la malalamiko kuhusu
mchakato wa uchaguzi ulivyokuwa kwa sababu hakuna fomu za malalamiko
zilizojazwa na kuwasilishwa tume kuanzia ngazi ya udiwani, uwakilishi na
nafasi ya urais wa Zanzibar.
Ayoub alisema hoja ya kutaka uchaguzi uhairishwe ilianza kujitokeza
Oktoba 26, mwaka huu baada ya viongozi wa CCM kuwasilisha malalamiko
yao na kutaka uchaguzi huo utangazwe ni batili na urejewe upya bila ya
kuonesha vielelezo vya kuharibika kwa uchaguzi huo.
Alisema waangalizi wa ndani na nje wakiwamo mawakala, wameridhishwa
na uchaguzi ulivyokwenda na mpaka juzi majimbo 31 yalikuwa yametangazwa
na kazi ya kukamilisha uhakiki wa majimbo 23 ulikuwa ukifanyika wakati
mwenyekiti akitoa uwamuzi huo wao makamishna walikuwa wakiendelea
kuhakiki matokeo ya uchaguzi huo. Wakizungumza kwa nyakati tofauti
makamishna hao, walisema wameshtushwa na mwenyekiti wa tume hiyo kufanya
maamuzi yake binafsi na kueleza uamuzi huo hawautambui na kumtaka
arejee kazini wakamilishe kazi iliyobakia na kumtangaza mshindi wa
uchaguzi huo.
Kuhusu nafasi ya urais baada ya uchaguzi huo kufutwa, Ayoub alisema
kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, “rais ataendelea kuwa
rais mpaka rais anayechaguliwa na kuapishwa, utaratibu huo
unapokamilisha,” alisema Ayoub.
Makamishna hao walikanusha hoja ya mwenyekiti juu ya kuwapo baadhi
ya makamishna waliovua mashati na kupigana kwa kutetea misimamo ya vyama
vyao na kusahau wajibu wao katika tume kama ilivyoelezwa katika sababu
tisa za kufutwa matokeo hayo.
“Hakuna watu waliopigana, Bunge la Kenya wabunge wake hufikia
kupigana, ufumbuzi hauwi kulivunja bunge, na chaguzi nyingi zimewahi
kutokea duniani na ufumbuzi huwa sio kufuta matokeo ya uchaguzi bali
kurekebisha kasoro,” alisema.
WAKILI MAHAKAMU KUU ZANZIBAR AIPINGA ZEC
Nassor Khamis, ambaye ni wakili mkongwe wa Mahakama Kuu ya
Zanzibar, alisema kwa mujibu wa utaratibu wa kisheria uliowekwa, huwezi
kupiga kura bila ya kuwamo katika orodha ya wapigakura na kushangaa
madai ya kuwapo kwa kura bandia zinazodaiwa kutumika kisiwani Pemba.
Alisema uamuzi uliofanywa na mwenyekiti utaleta matatizo makubwa
kikatiba kwa vile wapigakura wa Zanzibar ndio hao hao wapigakura
wanaochagua mbunge wa Jamhuri ya Muungano na rais na kama
kunaudanganyifu lazima uguse mchakato wa uchaguzi huo.
“Zanzibar haitakuwa na wabunge wa Jamhuri ya Muungano kwa sababu
wao ndio wanaopiga kura kuchagua rais wa Zanzibar, muwakilishi na
udiwani, mbunge na rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,”alisema.
No comments:
Post a Comment